Baada ya Dreamliner hapa ndipo ulipofikia ujenzi wa Reli ya kisasa (Standard Gauge)

Shirika la Reli la Tanzania limefanya kampeni ya kujengeana uelewa ndani ya taasisi hiyo pamoja na kufanya mawasilisho ya mradi wa ujenzi wa reli ulipofikia.

Akizungumza na waandishi wa habari Meneja wa Mradi wa Ujenzi wa Reli ya kisasa ya Standard Gauge, Engineer Maizo Mgedzi amesema kuwa hadi sasa hatua ya ujenzi wa reli ya kisasa kwa kipande cha Dar es Salaam-Morogoro kimefikia asilimia 16 na kiasi cha fedha Trilioni 1.21 kimeshalipwa kwa mkandarasi.

“Tunategemea tumalize Mungu akipenda mwakani mwezi November, lakini kwa sasa kazi ambazo zinaendelea ni ujenzi wa tuta (kukata milima na kufukia), kujenga makarvet na madaraja,” amesema Mgedzi.

Amesema kuwa tayari nguzo kubwa 24 zimeshajengwa kati ya nguzo 100 zilizotakiwa kujengwa katika daraja kubwa la Dar es Salaam.

“Mpaka sasa changamoto kubwa ni mlolongo wa kukamilisha taratibu za kutoa ardhi kwa wakazi tutakao waondoa katika maeneo tunayopitisha reli, tunaitatua changamoto hii kwa kutekeleza hilo zoezi kwa mujibu wa sheria, makadilio ya fidia yatazidi Bilioni 40,” amesema Mgedzi

Mratibu wa mradi wa Uboreshaji reli ya Kati ya Dar- Isaka, Mlemba Singo amesema katika kuboresha reli ya kati watang’oa vyuma vya reli Km 313 na kuweka vyuma vipya pamoja na kuboresha madaraja 393.

“Wananchi wajiandae tunategemea kutakuwa na ongezelo la speed wamezoea treni ya sasa inakwenda kwa makadilio ya Km 35 kwa saa, tunakwenda kuiboresha mpaka kuwa Km 70 kwa saa,” amesema Singo.
Sponsored by ZAMOTO MEDIA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini