SERIKALI KUCHUKUA HATUA ZA HARAKA KUNUSURU ZIWA BASSOTU KUJAA NA KUSABABISHA MAAFA KWA WAKAZI WA KARIBU NA ZIWA HILO | ZamotoHabari.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akiangalia namna Ziwa Basotu wilayani Hanang mkoani Manyara lilivyofurika na kuziba barabara katika eneo hilo alipofanya ziara mkoani humo.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akipimwa joto la mwili alipowasili Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara kwa ajili ya ziara wilayani Hanang kuangalia athari za kufurika kwa Ziwa Basotu na kuzingira makazi ya wanachi.
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akinawa mikono alipowasili Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara kwa ajili ya ziara wilayani Hanang kuangalia athari za kufurika kwa Ziwa Basotu na kuzingira makazi ya wanachi.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akizungumza na wananchi wanaoishi na kufanya shughuli zao karibu na Ziwa Basotu wilayani Hanang mkoani Manyara ambalo limefurika na kuharibu miundombinu.
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Hanang Mhe. Dkt. Mary Nagu alipofanya ziara katika Ziwa Basotu wilayani Hanang mkoani Manyara kujionea changamoto ya kufurika na kuzingira makazo ya wananchi wa eneo hilo na kuharibu miundombinu ya barabara.
Sehemu barabara ambayo imejaa maji yaliyofurika katika Ziwa Basotu wilayani Hanang mkoani Manyara na kusababisha mafuruki kwa wananchi wa eneoa hilo.
Mkuu wa Wilaya ya Hanang, Joseph Mkirikiti (kushoto) akifafanua jambo wakati wa ziara ya Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu katika eneo hilo la Ziwa Basotu lililofurika na kuzingira makazi ya wananchi na kuharibu miundombuni.

(PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)

*********************************

Mwandishi wetu, Manyara

Serikali imeahidi kuchukua hatua za haraka kunusuru Ziwa Bassotu wilayani Hananag mkoani Manyara kutokana na kujaa na kufurika maji ambayo yamezingira makazi ya wanachi wa eneo hilo.

Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu alipotembelea eneo hilo kujionea athari hizo zilizotokana na mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini.

Katika ziara hiyo akiwa ameambatana na wataalamu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) aliahidia kuwa Serikali itatumia wataalamu hao kufanya utafiti ili kupata suluhisho la kudumu.

Akizungumza na wananchi wa eneo hilo walioathirika na mafuriko aliwaahidi kuliweka suala hilo katika miradi ya Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa ajili ya kupata fedha zitakazosaidia kulitatua.

“Tumetazama tatizo hili hapa panahitaji utaalamu mkubwa tutachukua hatua kwani tunaona eneo lote la ziwa limeingiwa udongo na kufanya maji yafurike na tunaweza kudhani maji ni mengi kumbe wakati wa kiangazi tutakuwa na shida ya maji kwa hiyo kuweni na Imani na Serikali yenu tutalifanyia kazi,” alisema.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya hiyo, Joseph Mkirikiti alisema athari zilizotokana na mafuriko hayo ni uharibifu wa miundombinu ikiwemo nyumba za wakazi wa eneo hilo kuzingirwa na maji.

Aidha, Mkirikiti aliongeza kuwa sema kwa takriban wiki tatu sasa kumekatika mawasiliano kati ya eneo hilo na Haydom ambapo barabara iliyo kando mwa ziwa hilo haipitiki kutokana na kujaa maji.

Mkuu huyo wa wilaya aliomba mamlaka zinazohusika ziweze kuchukua hatua kwa wakati ili kunusuru wananchi hao wasipate madhara Zaidi kutokana na nyumba zao kuzingirwa na maji. Hata hivyo itakumbukwa hivi karibu iliagizwa barabara ya Haydom – Katesh isitumike ili kuepusha madhara kwa watumiaji kutokana na kufurika kwa maji hayo.

Akizungumza kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti na Hifadhi ya Mazingira wa NEMC, Lilian Lukambuzi alisema tatizo hilo limetokea kutokana na shughuli mbalimbali za binadamu. Lukambuzi alisema kuwa panapaswa kufanyika utafiti kama ambavyo Waziri alielekeza pamoja na kuweka mipango ya muda mfupi na mrefu kwa ajili ya kunusuru ziwa hilo.

Alisema kuwa moja ya hatua za haraka zinazopaswa kuchukuliwa ni pamoja na kuzuia shughuli za kibinadamu zinazofanyika katika maeneo hayo ambazo ndizo chanzo cha tatizo hilo. Naye Mbunge wa Jimbo la Hanang Mhe. Dkt. Mary Nagu alionesha hofu yake ya ziwa hilo kuweza kujaa udongo kutokana na mito inayotoka maeneo mbalimbali na hivyo kukosekana kwa maji.

Alimshuruku waziri huyo kwa kufika na wataalamu kutoka NEMC chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais na kujionea madhara mbalimbali yanayotokana na kufurika kwa mto huo hivyo kuwa tayari kuyafanyia kazi.

Kwa mujibu wa mbunge huyo, Ziwa Basotu ni chanzo kikubwa cha maji kwa wananchi wa Wilaya ya Hanang katika Mkoa wa Manyara


APP YETU MPYA: Sasa unaweza kusoma kwa urahisi kupitia APP yetu. Download hapa kwa KUBOFYA HAPA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini