WAUMINI WA DINI WATAKIWA KUENDELEA KUMTANGULIZA MUNGU WAKATI WAKIJIANDAA NA UCHAGUZI MKUU 2020 | ZamotoHabari.


Na Jumbe Ismailly IKUNGI .

WAUMINI wa madhehebu ya dini mbali mbali nchini wametakiwa kuendelea kumtanguliza Mungu wakati wakijiandaa na uchaguzi mkuu wa Rais,Wabunge pamoja na madiwani unaotarajiwa kufanyika Okt,28,mwaka huu.

Askofu Mkuu wa Kanisa la Internatinal Evangelism Church,Dkt Eliud Isanjya alitoa ushauri huo wakati wa ibada ya shukrani ya kutimiza miaka hamsini ya utumishi mtakatifu wa Askofu Jacob Nyika iliyofanyika katika kanisa hilo lililopo katika mji mdogo wa Ikungi,Mkoani Singida.

Aidha Dkt Isanjya alisisitiza kwamba kwa kuwa mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi na kampeni zinaendelea hivyo waumini wa madhehebu yota hayana budi kutambua umuhimu wa uchaguzi huo kuwa ni jambo kubwa sana linaloikabili nchi yetu.

“Huu ni mwaka wa uchaguzi na kampeni zinaendelea na pia uchaguzi ni mwezi wa kumi tarehe 28,hili jambo ni kubwa kwa nchi yetu na pia tungependa tumwambie mungu juu ya jambo hili lilivyo kubwa na pia umuhimu wake na jinsi ambavyo tusingependa tufanye wenyewe,bali tungependa tufanye na mungu.”alifafanua askofu mkuu huyo wa kanisa la Internatinal Evangelism Church.

Hata hivyo askofu mkuu huyo aliweka bayana kuwa ili uchaguzi huo uweze kufanyika kwa amani,utulivu na upendo ni wakati muafaka sasa wa kumkaribisha Mungu katika uchaguzi wa mwaka huu kwa kuhakikisha wanadumisha amani,upendo,utulivu na mshikamano uliopo miongoni mwao.

“Na si tukijua kwamba kwa miaka mitano au zaidi kwa uongozi mwingine tumeendelea katika nchi hii kwa amani,miaka hii mitano ambayo Mh Rais wetu Dkt John Pombe Magufuli ameongoza tumeona amani,tumeona pia maendeleo pamoja na mambo mazuri”alibainisha askofu Isanjya.

Kwa mujibu wa askofu mkuu huyo katika kipindi cha miaka mitano ambayo Mh Rais,Dkt John Pombe Magufuli aliyoongoza wameona amani,wameona pia maendeleo,wameona mambo mazuri,kwa hali hiyo wangependa uzuri huo na amani hiyo iendelee.

Akisoma wasifu wa askofu John Nyika,askofu Moses Mapunda kutoka Dar-es-Salaam aliyataja madhdumuni ya jubilee ni kutokana na utumishi mzuri uliotukuka wa askofu huyo katika kanisa la Internatinal Evangelism Church,hivyo kanisa likaona ni vyema kumpongeza kwa kutimiza miaka hamsini katika utumishi wake uliotukuka.

“Kutokana na hekima na busara alizonazo Baba Askofu Jacobo Nyika ushauri wake bado unahitajika kwenye kazi ya mungu kwa hiyo tunamuomba mungu ampe maisha marefu katika kumtumikia mungu na kutimiza kusudi lake hapa duniani.”alisisitiza.

Akizungumza na waumini wa kanisa hilo,Mkuu wa Mkoa wa Singida,Dkt Rehema Nchimbi alitumia fursa hiyo kukema suala la ukabila na makabila kwa kuwataka waumini hao kuondokana na dhana hiyo isiyofaa kwa wakati huu wa kampeni za uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Okt,28,mwaka huu. “Suala la ukabila na makabila uondoke ninasema hivi kwa sababu hata katika suala la uchaguzi huu watu wanaenda na ukabila,suala hapa siyo ukabila hapa ni Mungu aliyehai,na nathubutu kusema Mungu wa Magufuli..kama kuna mungu wa Elia,mungu wa Yakobo,mungu wa isaka,ni mungu wa Magufuli.”alisisitiza huku akishangiliwa kwa vigelegele na waumuni waliohudhuria ibada hiyo.
Ni baadhi ya wageni waalikwa na waumini waliohudhuria kwenye ibada ya shukrani ya kutimiza miaka hamsini ya utumishi mtakatifu wa Askofu Jacob Nyika iliyofanyika katika kanisa la Internatinal Evangelism Church lililopo katika mji mdogo wa Ikungi,Mkoani Singida.
Mkuu wa Mkoa wa Singida,Dkt Rehema Nchimbi akiwa katika ibada ya kumwombea Askofu Jacob Nyika kwa kutimiza miaka 50 ya utumishi mtakatifu.
Askofu Jacob Nyika (wa kwanza kutoka kushoto) akiwa na mke wake Mama Jacob Nyika wakati wa ibada ya shukrani ya kutimiza miaka 50 ya utumishi mtakatifu wakati katika Kanisa la Internatinal Evangelism Church.
picha ya pamoja ya Askofu Eliud Issangya (wa nne kutoka kulia waliosimama) akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida,Dkt Rehema Nchimbi aliyekuwa mgeni rasmi kwenye ibada hiyo(wa tatu kutoka kushoto waliosimama) pamoja na viongozi wengine wa serikali.(Picha zote Na Jumbe Ismailly)


APP YETU MPYA: Sasa unaweza kusoma kwa urahisi kupitia APP yetu. Download hapa kwa KUBOFYA HAPA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini