KIUNGO WA PSG APINGA VIKALI HARAKATI ZA MAPENZI YA JINSIA MOJA | ZamotoHabari


Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV

KIUNGO wa Kimataifa wa Senegal anayecheza katika Klabu ya PSG ya Ufaransa, Idrissa Gana Guaye amekuwa matatani baada ya kupinga harakati za Mapenzi ya Jinsia moja (LGBTQ Movement) nchini Ufaransa baada kugomea kuvaa Jezi zenye alama ya upinde wa Mvua (Rainbow) inayoashiria kuunga mkono harakati hizo.

Gana Guaye alikosa mchezo wa Ligi Kuu Soka nchini humo (Ligue 1) siku ya Jumamosi dhidi ya Montpellier ambapo PSG waliibuka na ushindi wa bao 4-0 dhidi ya timu hiyo. Kiungo huyo anayeamini katika maadili ya dini ya Kiislamu alikosekana katika mchezo huo sababu zikitajwa ni sababu binafsi.

“Hakuwa na majeruhi lakini ninachojua ni sababu zake binafsi, ndio maana tumemkosa katika mchezo wetu wa Jumamosi dhidi ya Montpellier”, amesema Kocha Mkuu wa PSG, Mauricio Pochettino akinukuliwa kupitia Mitandao mbalimbali.

Hata hivyo, Shirikisho la Soka nchini Ufaransa (FFF) kupitia Kamati yake ya Maadili imemtaka Kiungo huyo kueleza kwa nini alikosa mchezo huo wa Jumamosi dhidi ya Montpellier. Taarifa zinadai mwaka jana, Kiungo huyo alikataa kuunga mkono harakati hizo na alikosa mchezo kama huo dhidi ya Montpellier.

Rais wa Senegal, Macky Sall amemuunga mkono Kiungo Gana Guaye baada ya kuandika katika kurasa ya Twitter, “Imani yake ya dini ya Kiislamu lazima iheshimiwe”. Pia baadhi wameonekana kumuunga mkono kutokana na kitendo hicho na kupachapa ujumbe mahsusi (WeareallIdrissa) kumuunga mkono zaidi.

Ripoti ya mtandao wa African News umesema kuwa nchini Senegal kuna zaidi ya asilimia 90 za watu wanaoamini katika dini ya Kiislamu, ripoti hiyo imeeleza kuwa watu wanaojihusisha na Mapenzi ya Jinsia moja nchini humo wanakumbwa na adhabu ya mwaka mmoja au miaka mitano Jela.

Idrissa Gana Gueye alisajiliwa na PSG ya Ufaransa kwa ada ya uhamisho ya £30m mwezi Julai, 2019 akitokea katika Klabu ya Everton ya Uingereza.

Kiungo wa PSG, Idrisss Gana Guaye
 Wachezaji wa PSG wakishangilia moja ya bao katika ushindi wa bao 4-0 dhidi ya Montpellier, sehemu ya Jezi zao zikiwa na upinde wa Rainbow, mchezo huo Kiungo Idrissa Gana Guaye hakuwepo, sababu zikitajwa ni sababu binafsi.

 



Tembelea Website ya Nyimbo za Injili Africa. Pakua na Kusikiliza bure bila malipoBOFYA HAPA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini