YANGA SC BADO ALAMA SITA KUTANGAZA UBINGWA | ZamotoHabari

 

Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV
WANANCHI! Young Africans SC wamebakisha alama Sita pekee kutangaza Ubingwa wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara baada ya leo kupata alama tatu muhimu wa mabao 4-0 dhidi ya Mbeya Kwanza FC kwenye mchezo uliopigwa katika dimba la Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Young Africans SC endapo itashinda michezo yake dhidi ya Biashara United FC na Coastal Union FC watatangaza Ubingwa huo ambao waliukosa katika misimu minne iliyopita. Yanga SC wakishinda michezo hiyo miwili watafika alama 63 ambazo hazitaweza kufikiwa na timu yoyote ambayo inashiriki Ligi Kuu msimu huu, endapo Simba SC atashinda michezo yake iliyobaki atafika alama 68 pekee.

Kwenye mchezo wao dhidi ya Mbeya Kwanza, Yanga SC walijihakikishia ushindi kwa mabao ya Mshambuliaji Fiston Mayele dakika ya 34, Saido Ntibazonkiza dakika ya 38, Dickson Ambundo dakika ya 45+2 na Heritier Makambo dakika ya 74 ya mchezo huo.

Furaha kubwa ya Mashabiki wa Yanga SC ni kuona Mshambuliaji wao kinara, Fiston Kalala Mayele akifunga, na amefanikiwa kufunga katika mchezo huo kwenye dakika ya 34 akifungua ukurasa wa mabao manne ya timu hiyo.

Yanga SC watacheza michezo miwili ya kutangaza ubingwa endapo watashinda, watacheza na Biashara United FC katika dimba la CCM Kirumba, Mwanza na Coastal Union FC katika uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Hata hivyo, Yanga SC watakuwa na kibarua cha Nusu Fainali ya Michuano ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) Mei 28, 2022 dhidi ya Simba SC katika Uwanja huo huo wa CCM Kirumba jijini Mwanza.


Tembelea Website ya Nyimbo za Injili Africa. Pakua na Kusikiliza bure bila malipoBOFYA HAPA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini