SAKHO AING’ARISHA TANZANIA TUZO ZA CAF 2022 | ZamotoHabari



Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV

MSHAMBULIAJI wa Kimataifa wa Senegal na Klabu ya Simba ya Tanzania, Pape Ousmane Sakho ameing’arisha Tanzania katika Tuzo za Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF) 2022 mjini Rabat, Morocco baada ya kutwaa Tuzo ya bao bora la msimu kwa upande wa soka la Wanaume.

Sakho ameshinda Tuzo hiyo kwa bao lake alilofunga dhidi Asec Mimosas ya Ivory Coast kwenye mchezo wa hatua ya makundi ya Michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF CC), mchezo uliopigwa kwenye dimba la Benjamin Mkapa, Dar es Salaam, Februari 13, 2022.

Sakho alifunga bao hilo kwa mtindo wa ‘Acrobatic Kick’ kwenye dakika ya 12 ya mchezo baada ya kupokea Pasi safi ya krosi kutoka upande wa kulia wa Shomari Kapombe, bao hilo lilikuwa la kwanza kwa Simba SC kwenye ushindi wa bao 3-1 dhidi ya Asec.

Baada ya kupokea Tuzo hiyo, Mchezaji Sakho amewashukuru Watanzania, Wachezaji wote wa Klabu ya Simba, na watu wote wa Benki la Ufundi la timu hiyo waliompa nafasi kucheza kwenye mchezo huo.

Kwenye kinyang’anyiro hicho, Sakho amewashinda Wachezaji wa Wydad Casablanca ya Morocco, Zouhair El Moutaraji aliyefunga bao safi dhidi ya Al Ahly SC kwenye mchezo wa Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF CL) na Mshambuliaji wa Malawi, Gabadinho Mhango aliyefunga bao safi dhidi ya Morocco kwenye Michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON).


 

Tembelea Website ya Nyimbo za Injili Africa. Pakua na Kusikiliza bure bila malipoBOFYA HAPA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini