Mbaroni kwa Kkunyoa Nywele Mwanafunzi kwa Nguvu

Mbaroni kwa Kkunyoa Nywele Mwanafunzi kwa Nguvu
DAVID Mwaisaka (24), mkazi wa kitongoji cha Bondeni ‘B’ wilayani Kyela mkoani Mbeya, amekamatwa na polisi kwa tuhuma za kumteka mwanafunzi wa darasa la saba Shule ya Msingi kati (12) kisha kumnyoa nywele kwa nguvu.


Jirani wa familia ya mtoto huyo, Mbatumile Kyelu mkazi wa kitongoji cha Ipyana ‘B’, alisema walimuhoji mtoto huyo na kusema Juma pili wakati akiaenda kanisani alipofika kwenye kitongoji hicho alimkuta mtu asiyemfahamu, ambaye alimuomba amchukulie sahani na kigoda amuingizie ndani.

Alisema baada ya mtoto huyo kukubali kumuingizia ndani vitu hivyo, mtuhumiwa aliingia ndani na kufunga mlango kisha kutoa kisu akimtishia kumuua.

Baada ya hapo inadaiwa alitoa wembe na kumnyoa nywele za mbele ya kichwa na nyuma kisha akamueleza aondoke pasipo kuangalia nyuma.

Neema Nakajange, mama mzazi wa mtoto huyo, alisema akiwa na jirani zake walimuona mtoto amenyolewa nywele huku akiwa amechanganyikiwa na baada ya kumhoji, alisema alifanyiwa kitendo hicho na mtuhumiwa, hivyo waliamua kumuita mwenyekiti wa kitongiji ambaye aliitaarifu Polisi.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Ipyana ‘B’, Gibson Mwambiji, alisema alipigiwa simu na mzazi wa mtoto huyo akiweleza jinsi alivyofanyiwa, ndipo alipoenda Polisi kutoa taarifa na kupewa RB na kumuamuru ampe mwenyekiti kitongoji cha Bondeni ‘B’ ili wamkamate mtuhumiwa.

Alisema baada ya kufika walimpatia RB mwenyekiti wa kitongoji hicho na kwenda kwenye tukio siku ya Jumanne kisha mtoto kuitaja nyumba hiyo kuwa ndipo alipoonekana mtuhumiwa anayeishi hapo, hivyo kumkamata kisha kumpeleka polisi kwa uchunguzi zaidi.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya, Mussa Taibu, alithibitisha kuwapo na tukio hilo na kueleza kuwa Jeshi la Polisi linamshikilia mtuhumiwa kwa ajili ya upelelezi na endapo atabainika kuhusika, watamfikisha mahakamani.

Matukio ya aina hiyo yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara wilayani hapa, ambapo siku kadhaa zilizopita mtu mmoja alituhumiwa kuwanyoa nywele wanafunzi akidaiwa kuzipeleka kwa waganga wa kienyeji kwa ajili ya kupata utajiri.


Sponsored by ZAMOTO MEDIA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini