Marekani yawashtaki raia 12 wa Russia kwa kuhujumu uchaguzi 2016


Katika mashtaka mapya dhidi ya raia wa Russia yaliyofunguliwa Ijumaa na mwendesha mashtaka maalum, raia 12 wa Russia ambao ni maafisa usalama wa jeshi wameshutumiwa kuingilia kati uchaguzi wa urais 2016.

Mwendesha mashtaka maalum wa Marekani Robert Mueller na Naibu Mwanasheria Mkuu Rod Rosenstein wametangaza mashtaka hayo yamefanywa na washauri wa mahakama jijini Washington.

Watuhumiwa 11 kati yao walifunguliwa mashtaka kwa kushiriki katika hujuma ya kudukua kompyuta, kuiba nyaraka na kuzitoa kwa umma ili kuyumbisha uchaguzi.

Mtuhumiwa wa 12 amefunguliwa mashtaka ya kushiriki katika hujuma kompyuta ya taasisi iliyokuwa na jukumu la kusimamia uchaguzi, ikiwemo bodi za majimbo ya uchaguzi, mawaziri wa majimbo na kompyuta zinazogawanya software na teknolojia zinazotumiwa kusimamia uchaguzi,” Rosenstein amesema.

Raia hao wa Russia walikuwa wanafanya kazi katika vitengo viwili vya ujasusi vilivyo ndani ya jeshi la Russia, idara ya ujasusi ya nchi hiyo, kwa mujibu wa mashtaka hayo.

Mashtaka hayo yametolewa kabla ya mkutano wa Rais wa Marekani Donald Trump na Rais wa Russia Vladimir Putin utakaofanyika Helsinki Julai 16. Rosenstein amesema alimpa rais muhtasari wa tuhuma hizo dhidi ya majasusi wa Russia mapema wiki hii.

“Rais anafahamu kwa ukamilifu hatua iliyochukuliwa na Idara hii,” Rosenstein ameuambia mkutano wa waandishi wa habari.

Mwezi Februari, mwendesha mashtaka maalum alitangaza mashtaka dhidi ya mtandao mmoja wa Russia wa kampuni ya Troll, wafanyakazi 12 na mfadhili wao.
Sponsored by ZAMOTO MEDIA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini