Maandamano ya Mange Kimambi Yamuondoa Chadema, Atimukia CCM | ZamotoHabari.



Dodoma. Katibu mwenezi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wilaya ya Bahi mkoani Dodoma nchini Tanzania, Yuda Mbata amebwaga manyanga na kujiunga na Chama cha Mapinduzi (CCM).

Mbata ametangaza kujiondoa katika chama hicho leo Alhamisi Januari 2, 2020 akitaja mambo manne yaliyomkimbiza kutoka chama hicho kikuu cha upinzani.

Ameyataja mambo hayo ni kutelekezwa na chama alipokamatwa kuhusu kuandaa maandamano ya Mange Kimambi yaliyokuwa yafanyike Aprili 26, 2018 (hata hivyo hayakufanyika).

Jambo la pili anataja kuwa Chadema kilimtelekeza katika jimbo la Chilonwa wilayani Chamwino alikokwenda kuweka misingi ya chama.

"Lakini mengine kudhalilishwa na Mange akiniita ni Kibaka wa serikali na juhudi kubwa zilizofanywa na Rais John Magufuli katika kuwatumikia wananchi nimeona bora kumfuata katika chama chake," amesema Mbata.

Kiongozi huyo amesema mara nyingi chama kimekuwa kikiwashawishi kumuunga mkono Mange lakini walipoona nguvu ya mwanadada huyo imepungua wanatafuta njia nyingine.

Mwenyekiti wa Chadema wilaya ya Bahi John Mtyama amesema kuondoka kwa Mbata hakuna madhara ndani ya chama.

Mtyama amesema safari za siasa ni kama watu waendao pamoja ndani ya chombo lakini mmoja akishindwa na kushuka chombo kinaendelea.

Mwananchi
Tembelea Website ya Nyimbo za Injili Africa. Pakua na Kusikiliza bure bila malipo
BOFYA HAPA

Post a Comment

0 Comments

close
Banner iklan disini